Monday, September 13, 2010

Turudishe heshima ya Tanzania yetu

Saturday, 11 September 2010 14:56

0diggsdigg

Na Ramadhan Semtawa



TANZANIA ina historia ya kusimamia misingi ya utu pamoja na heshima na thamani ya utaifa wa watu wake. Heshima hii kubwa iliifanya Tanzania kufahamika duniani kote kuwa kisiwa cha amani katika bara (Afrika) lililojaa migogoro ya kisiasa na kijamii.



Waasisi wa taifa letu wakiongozwa na Baba wa Taifa, marehemu Mwalimu Julius Nyerere, walisimama kidete kuhakikisha kuwa sauti ya Tanzania ikitoka inakuwa na nguvu na uhakika, hasa katika kutetea haki za wanyonge na dunia iliisikia.



Wakati Tanganyika ikielekea kupata uhuru mwaka 1961, Mwalimu Nyerer alitoa sauti akitaka Afrika Kusini chini ya utawala wa kidhalimu wa makaburu, iondolewe katika Jumuiya ya Madola.



Mwalimu alimwandikia barua gavana wa Tanganyika kuweka bayana msimamo wake kwamba, serikali ya Makaburu isipofukuzwa katika jumuiya hiyo, ikipata uhuru Tanganyika haitajiunga.



Msimamo huo ulisikika na Afrika Kusini, iliondolewa katika Jumuiya ya Madola. Lakini, hata wakati wa vita baridi Tanzania ilikuwa na msimamo thabiti wa kufuata ilichoamini.



Ni Tanzania iliyokuwa ikiheshimika kutokana na msimamo wake thabiti wa kujitwisha jukumu la harakati za ukombozi Kusini mwa Afrika. Msimamo huu haukuwa jambo dogo, kwa nchi ambayo ilikuwa ni changa kukubali kujenga uadui na kuzitunishia misuli tawala dhalimu kama ile Makaburu.



Heshima na sifa ya Tanzania ilisambaa na hata mwaka 1987, Mwalimu akiwa amestaafu Baada ya kustaafu Urais Novemba 30, 1985, Mwalimu alijaribu kuonyesha msimamo huo wa Tanzania hasa alipoombwa kuongoza Tume ya Kusini (South Commission) mwaka 1986.



Huu ni msimamo ambao, ukifanya uchambuzi wa kina unapata dhamira kuu ambayo ni kutaka nchi ndogo zipiganie maslahi na haki zao dhidi ya mataifa makubwa. Ni msimamo wa kimapinduzi.



Lakini, pia vipo visa vya watu wachache waliongia nchini na kutaka kufanya hujuma na kutukana taifa letu. Mifano hai, ni kukakamatwa na kuadhibiwa jasusi wa Kingereza anayefahamika kwa jina la Clever, aliyekuwa akitumikia utawala dhalimu wa Ian Smith wa iliyokuwa Rhodesia ya Kusini sasa Zimbabwe.



Clever alitumwa kulipua kambi za wapiganaji wa Frelimo, ZANU-PF na nchi nyingine za kusini ambazo zilikuwa nchini na daraja la Salenda jijini Dar es Salaam, lakini alitiwa nguvuni.



Pia kipo kisa maarufu cha Mgiriki George Papurus ambaye alitamba mitaani akisema serikali yote ya Tanzania aliitia mfukoni mwake lakini akawekwa mfukoni yeye.



Hii ni mifano hai ambayo ilionyesha Tanzania iliweza kulinda heshima yake ndani na nje. Hakukuwa na mtu awe raia wa ndani au nje aliyeweza kuhujumu nchi hii kipuuzi.



Uzalendo ulikuwa juu kuanzia kwa Rais Nyerere, viongozi wenzake, vijana wa vyombo vya ulinzi na usalama na raia wote waliivaa nchi milini mwao. Lakini, haya yote yalitokana na uongozi wa juu kusimamia misingi ya utaifa.



Msukumo wa kuangalia historia hiyo, ni baada ya kuona matukio mawili ambayo yamenichefua na kuonyesha sasa nchi yetu imefikia hatua hadi ya kutemewa mate!



Kitendo cha raia wa Pakistan kuchana noti yetu ya sh 5,000 jijini Mwanza ni cha dharau ya hali ya juu kwa utaifa wetu. Hiki ni kitendo cha kidhalimu na tusi kubwa kwa nchi hii iliyojengwa juu ya miamba ya mashujaa.



Anachana noti yetu ambayo ni moja ya sifa na utambulisho wa taifa huru! Huyu ametukana uhuru na utaifa wetu. Mtu anayejaribu kutukana uhuru wetu hatuwezi kukaa naye na kumwambia samahani bwana, tuachie uhuru wetu, siku zote uhuru unalindwa kwa nguvu.



Watu kama hawa wanapaswa kuonyeshwa maana ya kupigania uhuru ili kesho akirudi kwao akasimulie kama Paparus alivyokutana na mkono wa vyombo vya dola hadi akamwaga chozi mbele ya Mwalimu Nyerer akisema alikuwa amelewa ndiyo maana alisema, "Serikali yote ya Tanzania iko mfukoni mwake."



Lakini, utashangaa kusikia raia huyu ameachiwa huru. Hii ni kwasababu siku hizi tuna tatizo kubwa la kuwa na baadhi ya wasimamizi wa vyombo vya dola wasio wazalendo.



Binafsi, niliposikia kitendo hiki hisia zangu zilikwenda mbali! Ni kitendo ambacho hakivumiliki. Haiwezekani wageni waje katika nchi yetu na kututukana. Yaani mafisadi wa ndani na wahujumu uchumi watutukane, halafu wageni nao waje watutukane.



Tukio la pili, ni la meneja wa Kiwanda cha Sukari cha Mtibwa, mkoani Morogoro (raia wa Afrika Kusini), ambaye siku zote amekuwa akiwanyanyasa wafanyakazi wazalendo wa nchi hii. Huwa najiuliza kwamba, hivi hawa wageni wanapata wapi jeuri ya kuwanyanyasa Watanzania?



Nimefurahi na nampongeza Rais Jakaya Kikwete kwa msimamo wake thabiti wa kizalendo, kwa kuingilia kati na kufanikisha meneja huyu kufukuzwa kiwandani hapo. Lakini, haitoshi anapaswa kufukuzwa kabisa katika nchi yetu.



Nasema hivyo kwasababu wawekezaji hao wa kutoka Afrika Kusini wamewanyanyasa sana ndugu zetu katika migodi ya madini na maeneo mengine ya uwekezaji.

Matatizo ya meneja huyo, yalikuwepo tangu wakati wa serikali ya awamu ya tatu, lakini kilio cha wananchi hawa hakikusika hadi sasa, Angalau sasa Rais Kikwete akaingilia kati, ndiyo maana nampongeza sana.



Mtu unajiuliza, hivi Makaburu tumewasahau hadi tukaanza kuwapa uhuru wa kumiliki uchumi wetu kiasi hiki?



Umefika wakati, tunataka heshima ya Tanzania irejee na watu wanaokuja nchini na wahujumu wa ndani walijue hilo. Lazima fikra za kizalendo zirejeshwe ili kuhakikisha wote wanaojaribu kuidhalilisha nchi yetu wachukuliwe hatua kulingana na uovu wao. Tumechoka kuona nchi yetu inakitemewa mate.



Aluta continua



0714897200:

mwanamapinduzi@yahoo.com

0 comments:

Post a Comment