Thursday, November 25, 2010

Mdahalo - Freeman Mbowe na Hamad Rashid Mohamed

Napenda kuchukua nafasi hii, kwa niaba ya Vox Media kuwatangazia kwamba Jumamosi hii, yaanii Novemba 27, 2010, kuanzia saa moja jioni hadi saa tatu usiku, tutakuwa na mdahalo kati ya Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe na Kiongozi wa Kambi ya Upinzani aliyemaliza muda wake, Hamad Rashid Mohamed, Mbunge wa Wawi (CUF), kuhusu masuala yahusianayo na kambi hiyo bungeni.

Mdahalo huo utarushwa moja kwa moja na Kituo cha Televisheni cha ITV (saa moja mpaka tatu usiku). Kwa kuwa kadi zilizopo ni chache, wengi wenu mnashauriwa kuwa kando ya televisheni zenu kwa ajili ya kushuhudia.
Karibuni na ahsanteni.

Serikali mpya isimamiwe

MOJA ya habari kubwa leo ni Baraza jipya la Mawaziri lililotangazwa jana na Rais Jakaya Kikwete, Ikulu, jijini Dar es Salaam.

Baraza la Mawaziri lenye jumla ya mawaziri 50 huku likiwa limefanyiwa mabadiliko ya kimuundo katika wizara mbalimbali zilizokuwepo awali, lilifafanuliwa jana na Rais Kikwete kuwa linalenga kurahisisha ufanisi wa utendaji kazi wa serikali yake.

Izingatiwe kuwa katika idadi hiyo mawaziri ni 29 na manaibu waziri ni 21, na baraza hilo limezidi kuwa kubwa zaidi kuliko lile lililopita ambalo lilikuwa na mawaziri 47.

Ikumbukwe kuwa aliyekuwa mgombea urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willibrod Slaa, alikuwa akilalamikia sana ukubwa wa baraza la mawaziri lililopita huku akianisha takwimu mbalimbali zilizoonyesha kuwa lilikuwa likiongeza gharama kubwa zisizo za lazima katika uendeshaji wa serikali.

Aidha, hoja hiyo ya Dk. Slaa ilikuwa ikiungwa mkono pia na wasomi, wanaharakati na watu wa kada mbalimbali huku wakisisitiza kuwa ni muhimu kuwa na serikali ndogo yenye tija na inayobana matumizi.

Kinyume cha kilio hicho cha wadau wa siasa na masuala ya kiutawala, tunasikitika kuona Rais Kikwete ameshindwa kuwa msikivu na kurudia kuunda baraza kubwa tena kuzidi hata lile la awali.

Tunajua kuwa hoja ya Rais Kikwete kuongeza wizara na mawaziri ni kurahisisha utendaji na ufanisi wa serikali yake kama alivyoeleza jana wakati anafafanua sababu za kuigawa wizara ya miundombinu kuwa wizara mbili za Ujenzi na Miundombinu.

Hata hivyo bado tunachelea kushawishiwa na hoja hizo za rais, kwani ukweli ni kwamba mawaziri si watendaji bali ni wanasiasa wanaofanya zaidi kazi ya kuratibu na kusimamia sera ambayo inaweza kufanywa na mawaziri wachache ili mradi kuwe na watendaji bora.

Kwa mantiki hiyo, tulitegemea badala ya Rais Kikwete kuongeza ukubwa wa Baraza la Mawaziri, angefanya mabadiliko ya mfumo wa utendaji na watendaji wenyewe ili kuwarahisishia kazi mawaziri wachache na kuokoa fedha za walipa kodi kwa manufaa ya wananchi.

Kwa dosari hiyo kubwa, ni matumaini yetu kuwa wadau mbalimbali na taifa zima, kila mmoja kwa wakati wake na kwa nafasi yake ataendelea kutimiza wajibu wa kumsihi mkuu huyo wa nchi kupunguza ukubwa wa baraza lake. Bado tunaamini ni msikivu na ataitikia kilio hiki mbele ya safari.

Pamoja na dosari hiyo, bado tunawasihi Watanzania wote kuipa ushirikiano mzuri serikali hiyo mpya iliyotangazwa jana kwani ipo kwa ajili ya kuwatumikia wananchi wote bila kujali itikadi na tofauti zetu mbalimbali.

Hivyo basi, tunatoa rai kwa chombo kikuu cha kuwakilisha wananchi na kuisimamia serikali (Bunge) kuhakikisha kuwa linashauri, kuifuatilia na kuisimamia serikali hiyo mpya ili iwajibike vizuri na kwa uadilifu wa hali ya juu kwa masilahi ya vizazi vya leo na vya kesho vya taifa hili.

Tunahitimisha kwa kuwataka wananchi wa kawaida na vikundi shinikizi, zikiwamo asasi zisizo za kiserikali (NG’Os na CSO’s) pamoja na asasi za kidini kuunga mkono rai hii ya kuipa ushirikiano serikali yetu pamoja na kuisimamia.

source : tanzania daima

Shitambala ajibu agizo la Dk. Slaa

WAKATI uongozi wa taifa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), ukikataa ombi la kujiuzulu kwa mwenyekiti wa chama hicho Mkoa wa Mbeya, Sambwee Shitambala, kwa kutokidhi vigezo vya katiba ya chama, mwenyekiti huyo amesisitiza hatakuwa tayari kurudi katika nafasi hiyo kwa sasa hadi hapo chama hicho kitakapomaliza kabisa uchunguzi wake.

Shitambala ambaye ni wakili wa kujitegemea alisema ataendelea kukaa nje ya cheo hicho ili kupisha uchunguzi huru dhidi ya tuhuma za rushwa zinazoelekezwa kwake lakini pia kulinda hadhi ya kazi yake ya kutetea haki za raia kupitia kada ya sheria.

Msimamo huo aliutoa jana jijini hapa wakati akizungumza na waandishi wa habari kujibu maagizo ya chama chake, ikiwa ni siku moja tu baada ya Katibu Mkuu wa chama hicho taifa, Dk. Willibrod Slaa, kulikataa ombi lake na kumsihi aendelee na uenyekiti.

Kwa mujibu wa barua ya Shitambala aliyokiandikia chama hicho na Tanzania Daima kupata nakala yake, sababu kuu nne ndizo zilizomfikisha kwenye uamuzi wa kujiuzulu wadhifa huo.

Miongoni mwa sababu hizo ni yeye kutupiwa lawama za kupokea rushwa kwenye uchaguzi wa ubunge Jimbo la Mbeya Vijijini pamoja na mkoa kukosa mgawo wa wabunge wa viti maalumu.

Alisema mbali na ukweli ulivyo juu ya mfumo uliotumika kupata nafasi za wabunge wa viti maalumu, wanachama na baadhi ya viongozi wa chama hicho mkoa wamekuwa wakitaka majibu, hali ambayo imekuwa ikimuweka katika wakati mgumu kwani hakuhusika katika mchakato huo.

Alisema katika hali ya kushangaza uongozi huo wa juu wa chama badala ya kufikiria kwa kina hoja hizo nzito na kuzitafutia majibu yanayoweza kuwatuliza wanachama wenye hasira wao wameendelea kutoa majibu mepesi.

“Hoja iliyopo mbele ni nzito, haiingii akilini Mkoa wa Mbeya kukosa nafasi ya viti maalumu wakati tumefanya kazi kubwa ya kukiinua chama tena kwa muda mfupi, walipaswa kutoa tiba kwanza kwa hili ndipo waamuru mimi nirudi kwenye nafasi yangu,” alifafanua Shitambala.

Aliongeza kuwa baada ya kupata nafasi ya kuwa mwenyekiti maisha yake yalitengenezwa katika sura mbili hivyo kitendo chake cha kuamua kujiuzulu kutokana na tuhuma za rushwa zinazotokana na mambo ya siasa kina lengo la kuokoa hadhi ya maisha ya upande wa pili wa taaluma yake ya sheria.

“Si rahisi mimi kuona maisha ya siasa yanaharibu maisha yangu ya kawaida na wala maisha yangu ya kawaida yakiharibu maisha ya siasa, ni vizuri nikaeleweka hivyo. Mimi bado ni mwanachama mwaminifu na punde yote haya yakishughulikiwa na mimi kuonekana sikuhusika basi nitarudi kuwatumikia wananchi,” alisisitiza Shitambala.

source : tanzania daima

Dk Slaa anena: Sitta akikubali, nitamshangaa

Fidelis Butahe
VIONGOZI wa vyama vya upinzani wameponda uteuzi wa Rais Jakaya Kikwete wa Baraza la Mawaziri, huku katibu mkuu wa Chadema, Dk Willbroad Slaa akisema atashangaa kama Samuel Sitta ataridhia uteuzi wake wa kuwa Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki ambao amesema utamshushia hadhi.

Sitta alikuwa amechukua fomu za kutaka achaguliwe tena kuliongoza Bunge la Jamhuri ya Muungano lakini CCM ikamuengua kwa kile ilichoeleza kuwa ni kutaka wanawake waongoze moja ya mihimili ya nchi.
Kuenguliwa kwake kulifanya wengi wabashiri kuwa Rais Kikwete angempa wizara nyeti kama ya Katiba na Sheria ili aongoze mabadiliko ya katiba baada ya Zanzibar, lakini jana alitangazwa kushika wizara hiyo ya ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Dk Slaa, ambaye aligombea urais kwa tiketi ya Chadema, alisema kuwa uteuzi wa Sitta umelenga kuendeleza ufisadi na kwamba iwapo spika huyo wa zamani ataikubali kushika nafasi hiyo, atakuwa amejishushia hadhi.
Dk Slaa, ambaye aligomea matokeo ya kura za uchaguzi wa rais na baadaye chama chake kutangaza kutotambua matokeo hayo, alisema: “Nilitegemea kusikia Baraza la Mawaziri 20 hadi 25. Sasa hawa mawaziri wote wanakwenda wapi, watapewa nyumba na magari ya Sh200 milioni, hivyo fedha nyingi zitatumika kwa matumizi yasiyo na ulazima.”
“Hili baraza limeundwa kujenga utawala wa kifisadi, kazi ya Baraza la Mawaziri si kumlinda rais ni kuwahudumia Watanzania; hizi si sura sahihi.”

Dk Slaa alisema kwa kiongozi makini kama Sitta kupelekwa Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki ni mwendelezo wa ufisadi na kusisitiza kuwa atamshangaa kama atakubaliana na uteuzi huo.
“Naelewa kilichomkumba Sitta... kila siku nasema hii kauli na sitachoka kuisema kwa kuwa naipenda nchi yangu. Inakuwaje unatoa nafasi za uwaziri kwa ajili ya kulipa fadhira? Hii si sahihi hata kidogo,” alisema Dk Slaa.
“Uteuzi wa Sitta kwenye wizara hiyo ndio utatudhihirishia kama kweli yeye ni mpambanaji wa ufisadi au la.”
Dk Slaa pia aliponda uteuzi wa William Ngeleja kuwa Waziri wa Nishati na Madini pamoja na Makongoro Mahanga kuwa Naibu Waziri wa Wizara ya Kazi na Ajira kuwa hauna mantiki.

Hata hivyo hakufafanua zaidi sababu za kauli yake hiyo kuponda mawaziri hao.
Mwenyekiti wa APPT-Maendeleo, Peter Mziray alisema kuwa baraza hilo halina jipya na akamshangaa Rais Kikwete kutumia siku nyingi kabla ya kutangaza baraza wakati hakuna jipya alilolifanya katika uteuzi wake.
“Watanzania wategemee maisha yaleyale tu, hakuna mabadiliko yoyote... labda kikubwa ni uteuzi wa (Waziri mpya wa Ujenzi, John) Magufuli na waziri mpya wa Ardhi, Nyumba na Makazi, Anna) Tibaijuka. Lakini, Tibaijuka naye hatakuwa na kazi rahisi kwa kuwa ndio mara yake ya kwanza anakuwa waziri na alikuwa ameshazoea kazi za kimataifa ambazo ni tofauti na za wizara,” alisema Mziray.

Alisema kwamba kuona baraza dogo lenye mawaziri wasiozidi 30 na kusisitiza kuwa uteuzi uliofanywa na Rais Kikwete unaendeleza mfumo wa CCM wa kupeana ulaji.
“Ili Watanzania waondokane na karaha hii, suluhisho ni kuwachagua wapinzani. Siku wapinzani wakiingia madarakani haya yote yatakwisha,” alisema Mziray.
Mwenyekiti wa DP, Mchungaji Christopher Mtikila alisema kuwa uteuzi huo umewapa watu ambao ni wagumu wa kufikiri matatizo na shida za Watanzania akipinga uteuzi wa Wazanzibar katika baraza hilo.
“Haiwezekani; Zanzibar wamevunja Muungano inakuwaje nao wanaingizwa katika baraza la mawaziri. Huku ni kujipendekeza kwa namna ya kipekee,” alisema Mtikila.

Mchungaji Mtikila ambaye alienguliwa katika kinyang’anyiro cha urais kwa madai ya kutokuwa na wadhamini katika mikoa 10 ya Tanzania Bara, alidai kuwa alichokifanya Rais Kikwete ni kuwafurahisha watu fulani ambao hakuwataja watu hao.

“Uteuzi huu si kwa ajili ya maslahi ya Watanzania; baraza hili la mawaziri ni maafa makubwa. Nchi ya Ujerumani ina mawaziri 14, Marekani hawazidi 30, lakini sisi ndio tunaendeleza kufurahishana. Nakwambia baada ya miaka mitano nchi hii itakuwa imekwisha kabisa,” alisema Mchungaji Mtikila.
Naye mwenyekiti wa TLP, Augustine Mrema alisema Kikwete anatakiwa kuwa mkali kwa baraza hilo ili mawaziri wake wasifanye mzaha.

“Yaani hawa mawaziri naona wangekuwa na barua za kujiuzuru mkononi ili watakapovurunda iwe ni kukabidhi barua hizo na kuachia ngazi. Ni kweli baraza ni kubwa, lakini kama kutakuwa na uwajibikaji, sidhani kama kutakuwa na tatizo, ila kama wakilala, hapo ndio mambo yatakapoanza kuwaharibikia,” alisema Mrema.
Mrema alimpongeza Rais Kikwete kwa kuwateua Magufuli na Anna Tibaijuka akisema kuwa ni watendaji wazuri.

SOURCE : MWANANCHI

Monday, November 22, 2010

Dk Bana: Chadema wana hoja ya msingi

Sadick Mtulya
MKUU wa Idara ya Sayansi ya Siasa katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk Benson Bana, amesema Chadema kina hoja ya msingi kushinikiza uundaji katiba mpya na kwamba, tatizo lipo njia wanayotumia.
Kauli ya Dk Bana inakuja ikiwa ni siku chache, baada ya wabunge wa Chadema kutoka nje ya ukumbi wa Bunge wakati Rais Jakaya Kikwete akianza kuhutubia, kuashiria kuzindua rasmi.

Chadema ilifaya hivyo ikiwa ni hatua yao kupinga matokeo ya urais yaliyotangazwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) na kushikiza uundaji wa katiba mpya, Nec na uundaji Tume ya uchunguzi wa yaliyoajiri uchaguzi mkuu uliopita.
Kufuatia kitendo hicho, wasomi, wanasiasa, viongozi wa dini na wananchi waliibuka na maoni tofauti.
Akizungumza katika kipindi cha ‘Tuongee Siasa’ kupitia Kituo cha Televisheni cha Star Tv jana, Dk Bana alisema madai ya chama hicho yana msingi.
“Madai ya Chadema ni ya msingi, lakini tatizo ni njia waliyotumia kutozingatia utamaduni wa Watanzania katika kudai haki,’’ alisema.

Dk Bana alisema Chadema imetumia njia hasi ambayo kimantiki itajenga tabia kwa wananchi wa kada tofauti kususia vikao au mikutano itakayokuwa inaitishwa na viongozi.
“Kama njia hii itakubalika katika jamii, itafikia hatua hata wanafunzi watatoka nje ya darasa wakati mwalimu akiwa anafundisha, kwa hoja kwamba hawamtaki jambo ambalo ni kinyume na maadili ya Watanzania na hatari kwa mustakabali wa baadaye wa taifa,’’ alisema.

Kuhusu Katiba, alifafanua kwamba kulingana na mabadiliko ya wakati, Katiba ya sasa ambayo ilitungwa mwaka 1977, haikidhi haja na tija ya Watanzania inastahili kutungwa upya.

“Kulingana na wakati, inahitajika katiba mpya itakayokidhi haja na tija kwa Watanzania wote, Katiba ambayo itatoa fursa zaidi kwa wananchi kuweza kuwajibisha viongozi,” alisema na kuongeza:
“Itatoa fursa ya kujadiliwa zaidi kwa masuala ya muundo wa muungano, uteuzi wa mawaziri, uteuzi wa watendaji wakuu wa taasisi za serikali, uwepo wa tume huru ya uchaguzi, rais kupunguziwa madaraka na mambo mengine.’’

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, amenukuliwa akisema uamuzi wao ulizingiatia demokrasia na kwamba, ulipeleka ujumbe mzito kwa Watanzania na Jumuiya ya Kimataifa ili kuibua mjadala wa kitaifa juu ya umuhimu wa masuala hayo matatu.

chanzo : gazeti mwananchi

Chadema: Tuko tayari kukaa mezani na serikali

Sunday, 21 November 2010


Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe

Mwandishi Wetu

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimesema kipo tayari kukutana na serikali, chama au taasisi nyingine yoyote itakayotaka kujadiliana kuhusu hatua yao ya kutoyatambua matokeo ya uchaguzi wa urais na madai yao ya katiba mpya.

Katika tamko ambalo halijawahi kutokea kwenye siasa za Tanzania, Chadema ilitangaza kuwa haitambui matokeo ya uchaguzi wa rais kwa madai kuwa taratibu nyingi zilivurugwa kwa lengo la kumbeba mgombea wa chama tawala na ilidhihirisha msimamo wao wakati wabunge wa chama hicho walipotoka kwenye ukumbi wa Bunge mara baada ya Rais Jakaya Kikwete kuanza kuhutubia.

Lakini jana mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe aliiambia Mwananchi kuwa wako tayari kukaa meza moja na serikali au taasisi ambayo wataiona kuwa inaweka mbele maslahi ya taifa ili kujadiliana nayo kuhusu msimamo huo wa kwanza kuweka dhidi ya rais wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano. Msimamo wa Chadema umetolewa wakati mwandishi msaidizi wa rais, Premi Kibanga akikitaka chama hicho au Mbowe kufuata taratibu zilizopo iwapo wana lengo la kweli la kutaka majadiliano.

Kibanga alisema kuwa Mbowe, kama mwanasiasa na kiongozi wa kitaifa, anazifahamu taratibu na njia za kutumia iwapo anataka kukutana na serikali. Lakini mbunge huyo wa Hai alisisitiza kuwa hawangependa majadiliano yao ya serikali yachukue sura ya kisiasa kwa kuwa kufanya hivyo hakutafanikisha kufikiwa kwa lengo wanalolikusudia. “Lengo letu ni kuhakikisha kuwa tunalifikisha taifa hili mahali ambapo amani na utulivu utaendelea kuwepo.


Kati ya madai yetu yote hakuna jambo ambalo ni kwa ajili ya Chadema... tunayoyadai yatainufaisha CUF, CCM, vyama vingine vya siasa na wananchi wote,” alisema. Hata hivyo, Mbowe alionya kuwa mazungumzo hayo yasitawaliwe na aina ya maoni yanayotolewa na viongozi kadhaa wa CCM, yakiwemo ya katibu mkuu wa chama hicho tawala, Yusuf Makamba na katibu wa itikadi na uenezi, John Chiligati. “Hawa wameonekana kuzungumzia suala hili kisiasa zaidi wakati lengo letu sisi si kupiga siasa. Angalia hata mambo wanayosema eti tutaleta hoja ya kuwafukuza Chadema bungeni... hoja kama hiyo haina msingi kwa sababu hawana ubavu kisheria wa kufanya hivyo,” alisisitiza.

Alisema mazungumzo wanayoyalenga ni yale yatakayohakikisha kuwa madai yao yanafikiriwa kwa kina huku maslahi ya taifa yakiwekwa mbele. Alisema wanafurahi kuona kuwa kitendo chao cha kutoka bungeni wakati wa hotuba ya Rais Kikwete kimesaidia kuibua mjadala mzito nchini ambao iwapo utapewa nafasi ya kujadiliwa bila kuweka ushabiki wa kisiasa, nchi inaweza kupata mabadiliko makubwa siku za usoni.

Alitoa mfano wa wa watu kama waziri mkuu wa zamani, Jaji Joseph Warioba na Jaji Mkuu Augustino Ramadhani ambao walikaririwa wakisema kuwa suala la kuwa na katiba mpya ni muhimu. “Maoni kama haya, ambayo yanatoka kwa watu wazito kama hawa, yanaonyesha kuwa kitendo chetu kimeamsha mjadala wa maana kwa taifa hili,” alisema.

Alipoulizwa iwapo kitendo chao cha kutaka kukutana na serikali hakiathiri uamuzi wao wa kutotambua matokeo ya urais, alisema kuwa walishatamka tangu awali kuwa hawakatai kuwa kuna rais ingawa wanachopinga ni jinsi alivyopatikana. “Tunajua kuwa Kikwete ndiye ametangazwa kuwa rais, lakini tunachopingana nacho ni jinsi alivyoelezwa kuwa ameshinda katika uchaguzi... tunachokidai si kuwa uchaguzi urudiwe au kwamba Dk (Willibrod) Slaa atangazwe rais, la hasha. Tunalenga kuwa na mfumo bora siku za usoni ambao hautaacha shaka kwenye matokeo ya urais,” alisisitiza.


Alisema ni hatari sana kuwa na sheria ambayo hairuhusu watu kuhoji matokeo ya kura za urais katika mazingira ambamo watu wengi wanaingia kwenye kinyang’anyiro hicho. Alisema kuwa sheria ya kukataza kuhoji matokeo ya urais ilitungwa wakati wa mfumo wa chama kimoja wakati kukiwa hakuna mgombea wa kutoka vyama vya upinzani. “Wakati ule Mwalimu Nyerere ndiye kila mara alikuwa mgombea pekee, alikuwa hashindani na mtu yeyote kwa hiyo hakukuwa na mtu wa kuhoji. Wenzetu hawa wameichukua sheria hiyo na kuileta kwenye mfumo wa vyama vingi. Hauwezi kuitumia sheria hiyo hiyo wakati huu wa ushindani,” alisema.


Alisema iwapo matokeo ya uchaguzi wa ubunge na udiwani yanaweza kupingwa mahakamani, hakuna misingi ya kidemokrasia ya kukataza kupinga matokeo ya uchaguzi wa urais. Alitaka serikali kuiga mfano wa Senegal ambayo ina mahakama ya katiba ambayo moja ya majukumu yake ni kusikiliza malalamiko yote kuhusiana na uchaguzi wa rais na kiongozi mpya wa nchi haapishwi hadi mahakama hiyo imethibitisha matokeo hayo. Alisema pamoja na madai ya katiba mpya, madai yao mengine ambayo wangependa yajadiliwe iwapo watakutana na serikali ni kuundwa kwa tume huru itakayochunguza matukio yote kuhusu uchaguzi wa rais.

Alisema kwa mazingira yaliyopo, tume hiyo inaweza kuundwa na Rais Kikwete lakini kwa kuwachagua watu makini ambao wanaheshimika nchini. “Watu kama hao wapo wengi tu,” alisema.

Alionya kuwa si vema tume hiyo ikachukua mrengo wa kisiasa kwani kufanya hivyo kunaweza kupotosha majadiliano. “Kuna nafasi ya Chadema au CCM kuunda tume hiyo, lakini itaonekana kuwa ni ya kichama zaidi. Pia kuna nafasi ya Bunge kuunda tume, lakini Bunge nalo lina wanasiasa ambao wana maslahi kutoka katika vyama vyao. Hii ndiyo maana tunashauri rais anaweza kuunda tume hiyo lakini kwa kuhakikisha kuwa anawateua watu ambao wanaheshimika katika jamii ambao kila mmoja anajua kuwa wanajali zaidi maslahi ya taifa,” alisema.

CHADEMA Special Seats MP from Kigoma Hon. Mhonga S. Ruhwanya with Malaysian ex PM Tun. Dr. Mahathir Mohamad

CHADEMA Special Seats MP from Kigoma Hon. Mhonga S. Ruhwanya with Malaysian ex PM Tun. Dr. Mahathir Mohamad after a discussion in his Office at Petronas Twin Towers, Kuala Lumpur.