Sunday, November 14, 2010

Wanawake mliochaguliwa saidieni taifa - TAMWA

CHAMA cha Waandishi wa Habari Wanawake (TAMWA), kimewataka wanawake waliochaguliwa katika nafasi mbalimbali za uongozi mwaka huu wajiwekee malengo ya kuwatumikia kwa bidii, ubunifu, uadilifu na ujasiri mkubwa wananchi bila kujali itikadi.

Wanawake hao ni Anna Makinda aliyechaguliwa kuwa Spika wa Bunge, wanawake waliochaguliwa kuwa wabunge na madiwani kupitia majimboni na Viti Maalumu.

Taarifa iliyotolewa jana kwa vyombo vya habari mjini Dar es Salaam na kusainiwa na Mkurugenzi wa TAMWA, Ananilea Nkya, ilisema Spika Makinda ni mwanamke mwenye busara, msimamo thabiti, hekima na ujasiri na kwamba atatoa uongozi mpya wenye mtazamo wa kijinsia unaojali zaidi masilahi ya taifa na wananchi wengi.

“Tuna imani Bunge hili jipya chini ya uongozi wa mwanamke litaonyesha mfano kwa vitendo kwamba katika mfumo wa vyama vingi vya siasa inawezekana kuweka mbele masilahi ya wananchi na taifa kuliko masilahi ya vyama vya siasa au viongozi au mbunge mmoja mmoja.

“Ni matarajio yetu makubwa pia kwamba Spika Makinda atajenga mazingira mazuri yatakayoliwezesha Bunge lijalo kufanikisha taifa letu kupata katiba mpya ambayo pamoja na mambo mengine katiba hiyo itachochea uwajibikaji wa viongozi katika ngazi mbalimbali na kujituma kwa wananchi kufanya kazi kwa bidii ili kujenga taifa jipya lenye kujitegemea,” ilisema taarifa hiyo.

Makundi hayo ni pamoja na wanawake wasio na uhakika wa kipato mijini na vijijini, vijana wa kike na wa kiume waliokata tamaa ya maisha, watu wenye ulemavu, wajane na watoto yatima wanaonyang’anywa haki zao, watu wanaoishi na virusi vya ukimwi na wazee.

Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment